پایگاه اطلاع رسانی آیت الله ابراهیم امینی قدس سره

Madhumuni ya ndoa

Ndoa ni haja ya kawaida kwa kila mwanadamu. Inayo manufaa mengi na mazuri, baadhi ya hayo manufaa mengi na mazuri yaliyo muhimu ni haya: Ujengaji wa familia ambayo kwayo mtu anaweza kupata usalama na utulivu wa akili. Mtu ambaye hakuoa au kuolewa hufanana na ndege asiye na kiota. Ndoa hutoa huduma ya hifadhi kwa kila mtu anayehisi amepotea kwenye maisha yasiyo na mpango; mtu anaweza kupata mwenzi wa maisha ambaye anaweza kushirikiana naye katika furaha na huzuni.

Matamanio ya kawaida ya kijinsia yana nguvu na yenye maana. Kila mtu anatakiwa kuwa na mwenzi kwa lengo la kujitosheleza kijinsia kwenye mazingira yaliyo salama na tulivu. Kila mtu anapaswa kufaidi raha mustarehe ya kijinsia katika namna iliyo sahihi na inayostahiki. Wale wanao jiepusha na ndoa mara kwa mara husumbuliwa na maradhi ya kimwili na kisaikolojia.

Maradhi hayo na matatizo fulani ya jamii ni matokeo ya moja kwa moja ya vijana kujiepusha na ndoa.

Uzazi: Kupitia kwenye ndoa, binadamu wanaendelea kuzaana. Watoto ni matokeo ya ndoa na ni vipengele muhimu katika kuimarisha misingi ya familia na halikadhalika kama chanzo cha furaha kwa wazazi wao. Msisimko mkubwa sana umebainishwa kwenye Qur’ani Tukufu na Hadith kuhusu ndoa na kupata watoto. Mwenyezi Mungu Mweza wa yote anasema kwenye Qur’ani Tukufu:

    وَمِنْ آیَاتِهِ أَنْ خَلَقَ لَکُمْ مِنْ أَنْفُسِکُمْ

“Na katika Ishara zake ni kuwa Amekuumbieni wenza kutokana na nafsi zenu...” (Quran 30:21).

Mtume (s.aw) alisema: “Hapana muundo ulio bora zaidi ulio asisiwa katika Uislamu kuliko ndoa.”

Imam Ali (a.s) alisema: “Shiriki katika ndoa; kwa sababu hii ni Suna ya Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w).”

Mtume wa Mwenyezi Mungu (s.a.w.w) alisema: “Yeyote anayefuata Suna yangu lazima aowe na kuzaa watoto ambao ni matokeo ya ndoa na kuongeza umma wa Waislamu ili kwamba katika Siku ya Ufufuo nitakabiliana na umma wa mataifa mengine nikiwa na idadi kubwa ya umma wangu.”

Imam Ridha (a.s) alisema: “Mafanikio makubwa sana ya mtu ni kuoa mke mwaminifu, ambaye kila amuonapo anafurahi na hulinda mali yake na heshima yake mwenyewe wakati akiwa hayupo.”

Kilichozungumziwa katika sura hii kwa upande wa ndoa ni mambo yahusuyo dunia na maumbile tu ambayo pia wanyama wanayo; manufaa ya urafiki na kuzaana.

Kama ilivyo madhumuni ya kweli ya ndoa kwa jamii ya binadamu ni ya aina tofauti. Binadamu hakukusudiwa kuingia katika dunia hii kwa sababu ya kula, kunywa, kulala, kutafuta starehe au kuendekeza ashiki na halafu kufa na kuharibika. Hadhi ya mwanadamu ni ya juu zaidi kuliko matendo kama hayo. Wanadamu wanakusudiwa kujifunza wenyewe na roho zao katika kupata ujuzi, kufanya matendo mema na kuwa na tabia njema. Binadamu amekusudiwa kuchukua hatua kwenye njia iliyonyooka ili apate ukaribu wa Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.

Mwanadamu ni kiumbe ambacho kinaweza kusafisha roho yake kwa kuepuka matendo maovu na kujizoeza kuwa na tabia njema hufikia kiwango cha hadhi ya juu sana ambayo kwamba hata malaika hawezi kuipata.

Binadamu ni kiumbe ambacho ni cha milele. Amekuja hapa duniani ili kwa mwongozo wa manabii na utekelezaji wa utaratibu uliowekwa na dini ya Uislamu, aweze kupata furaha yake hapa duniani na Peponi, ili kwamba aweze kuishi maisha ya amani katika dunia ijayo daima milele.

Kwa hiyo, madhumuni ya ndoa lazima yatafutwe katika muktadha huu wa kiroho. Lengo la ndoa kwa mtu wa dini lazima iwe ni njia ya kuepusha matendo maovu na kutakasa roho kutokana na madhambi. Lazima iwe ni njia ya kupata ukaribu kwa Mwenyezi Mungu Mweza wa yote. Ni katika muktadha huu kwamba mwenza anayefaa na mwema huchukua jukumu muhimu.

Waumini wawili wanapounda familia kupitia katika ndoa, uhusiano wao wa kijinsia utawanufaisha katika kuimarisha mapenzi na wema wao, kwa wanandoa wa aina hiyo hapangekuwepo na hatari ya kutishia potovu wa kijinsia, mazoea mbaya au matendo ya haramu. Mtume (s.a.w) wa Uislamu na Maimamu wote (a.s) wamesisitiza sana kuhusu taasisi hii ya ndoa.

Mtume (s.a.w.w) alisema: “Yeyote anayeoa amelinda nusu ya dini yake.”

Imam Sadiq (a.s) alisema: “Rakaa mbili za Swala ya mtu aliyeoa ni zaidi ya rakaa sabini za Swala ya mtu ambaye hakuoa.”

Mumini mchamungu na mwenzi mpatanifu hutekeleza jukumu la maana sana katika kupata na maisha ya kuheshimika na kuaminika.

Kwa kweli kuwa na mwenzi wa aina hii ni kipengele muhimu kwa mtu anapotaka kuepuka matendo maovu na kuwezesha msimamo wa mtu katika kutekeleza matendo ya wajibu ya ibada.

Wanandoa wachamungu, si tu kwamba hawatakutana na vikwazo vyovyote katika kufanikisha malengo ya kidini, bali watakuwa chanzo cha kutiana moyo wenyewe kwa wenyewe.

Je, inawezekana kwa mtu muumini wa Mwenyezi Mungu kupigana kwa utukufu katika njia Yake bila ya uthibitisho wa mke wake? Je, inawezekana mtu yeyote mchamungu kupata riziki yake kihalali, kwa kuzingatia vipengele vyote vya kidini, kulipa sadaka iliyoamriwa kisheria ili kuepuka ubadhirifu, na kutumia katika kutoa msaada bila ya idhini ya mkewe?

Mchamungu kila mara angemlingania mwenzi wake kwenye wema, kama vile ambavyo mtu mpotovu angemshawishi mwenzi wake kuwa mpotovu.

Halafu ni jambo la maana kwamba kwenye Uislamu wanamume na wanawake ambao wanataka kuoa au kuolewa wanashauriwa kuangalia usafi na tabia njema za wale wanaotaka kuwa wenzi wao katika maisha ya ndoa, kama masharti ya muhimu.

Mtume (s.a.w.w) alisema: “Kama ingetokea mimi nimpe mtu Mwislamu mazuri ya dunia na akhera, ningemjalia moyo wa unyenyekevu, ulimi ambao ungetamka sifa Zake mfululizo, mwili wenye kuvumilia maafa yote, na ningempa mwenza katika ndoa mchamungu ambaye akimuona tu anafurahi, na analinda mali yake na heshima yake mwenyewe asipokuwepo.”

Mtu mmoja alikwenda kwa Mtume na akasema: “Ninaye mke ambaye hunikaribisha nyumbani kila ninaporudi na hunisindikiza hadi mlangoni ninapoondoka.

Anaponiona mimi nimehuzunika na sina furaha, kwa kuniliwaza na husema: ‘Kama unafikiria kuhusu riziki, basi usikate tamaa, kwa sababu Mwenyezi Mungu ndiye anayetoa riziki na kama unafikiria maisha yajayo, basi Mwenyezi Mungu na akuongeze akili yako na jitihada zako.’ Halafu Mtume (s.a.w.w) akasema; “Hakika Mwenyezi Mungu anao watendaji na wawakilishi hapa duniani na mke ni mmojawapo. Mwanamke wa namna hii atazawadiwa thawabu nusu ya mtu aliyejitolea mhanga.”

Imam Ali (a.s) alikuwa anafikiria haya haya aliposema kuhusu Hadhrat Zahra (a.s). Alisema kwamba mkewe alikuwa msaada mkubwa katika kumcha Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.

Historia inatuambia kwamba, siku moja kipindi kifupi baada ya harusi ya imam Ali (a.s) na Hadhrat Zahra (a.s), Mtume (s.a.w.w) alikwenda kuwapongeza nyumbani kwao na kujua hali yao. Alimuuliza Imam Ali (a.s): “Unamuonaje mkeo?” Imam akajibu; “Nilimuona Zahra kama msaada mzuri sana katika kumuabudu Mwenyezi Mungu Mweza wa yote.

Halafu Mtume aliuliza swali hilo hilo kwa Zahra (a.s) naye alijibu: “Mwenzangu ni mume mzuri sana.”

Katika sentensi moja, Imam Ali (a.s) alimtambulisha mwanamke bora katika Uislamu na akaelezea madhumuni makuu ya ndoa.